Habari, Makala na Simulizi kutoka Afrika

Mgogoro waibuka Hifadhi ya Jamii Burunge baada ya kitalu cha uwindaji kutangazwa bila ridhaa ya Viongozi

burunge wma

Mgogoro umeibuka katika Jumuiya ya Hifadhi ya Jamii (WMA), Burunge, wilayani Babati Mkoani Manyara baada ya kitalu kilichopo kwenye mapito ya wanyama kutangazwa kwa kampuni za uwindaji.

Tangazo hilo linataka kampuni kuwekeza upya kwenye shughuli za uwindaji kuanza January 2023.

Uwindaji ulisitishwa baada ya kamouni iliyopo sasa kuamua kufanya utalii wa picha pekee.

Hata hivyo, inadaiwa kuwa spika wa Jumuiya Hiyo ya Burunge WMA ametangaza kuwa kitalu cha uwindaji katika hifadhi ya jamii kipo wazi na kwamba kamouni yeyote inaweza kuwekeza katika shughuli hizo.

Hata hivyo bodi ya wadhamini katika hifadhi ya jamii ya Burunge inadai kuwa hawakushirikishwa katika utoaji wa maamuzi hayo.

Wakati spika wao akiwa amesaini barua ya kutangaza Kitalu hicho kutaka kampuni kuomba kuwinda  tayari Bodi ya wadhaini wa jumuiya hiyo imekwisha saini Mkataba kuendelea na  mwekezaji kampuni ya uwindaji wa kitalii ya EBN.

Mkataba huo ulihuisha tarehe 14 Julai 2022.

Kampuni ya uwindaji ya EBN ingawa ina kibali hicho lakini kwa muda sasa ilisitisha shughuli za uwindaji ili kuwezesha wanyama kuzaliana na kurejesha idadi yao ya awali.

“Tukumbuke kuwa haya ni mapito ya wanyama,” wanasema viongozi wa Burunge WMA.

Shoroba ya Kwakuchinja huunganisha hifadhi za Tarangire na Ziwa Manyara.

“Tunaona kuwa shughuli za uwindaji hapa katikakati zitaathiri mapito, hasa kipindi hiki ambacho serikali inajitahidi kufufua shoroba kote nchini,” inaongeza taarifa kutoka kampuni ya EBN.

Tayari Mkataba baina ya jumuiya ya hifadhi na mwekezaji wa awali umesainiwa na Mwenyekiti wa bodi ya wadhamini, Patricia Mosea, Katibu wa Burunge WMA, Benson Mwaise na Mkurugenzi wa EBN, Nicolas Negre.

Hii ni baada ya kutolewa baraka na Wizara ya Maliasili na Utalii baada ya tathimini na viongozi serikali  na halmashauri ya Babati.

Hata hivyo, inasemekana kuwa Spika wa Jumuiya hiyo, Hamis Juma amekuwa akitaka Kitalu hicho, kinachopakana na hifadhi ya Tarangire kupewa Kampuni ya nyingine ambayo sasa itafanya shughuli kamili za uwindaji.

Juma anadai kuwa kitalu cha uwindaji kipo wazi kwa uwekezaji mpya.

Akizungumza na Taifa Tanzania, Juma alikiri kuwepo na mgogoro katika jumuiya hiyo hata hivyo hakueleza au kufafanua kuhusu mvutano baina yake na Bodi ya wadhamini au Sekretarieti ya jumuiya hiyo ya uhifadhi.

Juma anaongeza kuwa tayari sakata hilo limekwisha kufikishwa kwenye ngazi za juu huku akisisitiza mkataba uliosainiwa awali na viongozi wa jumuiya ulikuwa na mapungufu.

Mmoja wa wajumbe wa bodi ya Burunge WMA anasema kuwa sio sahihi kutangaza kwamba kitalu cha hifadhi ya jumuiya kipo wazi wakati tayari eneo hilo lina mwekezaji halali.

“Sisi tunafurahia kwamba pamoja na kwamba ana kibali ya uwindaji, lakini amesitisha shughuli hizo na hivi sasa wanyama wanaongezeka kila siku,” alisema.

“Kwenye ule mkataba tuliosaini upo wazi kuwa kama tulitaka kuchukuwa Kitalu tunapaswa kutoa taarifa miezi mitatu kabla kwa kuwa kuna uwekezaji pale na tayari kuna watalii wamelipa Sasa anatumiwa na watu kutuvuruga na kuvuruga Utalii,” aliongeza.

Alisema tayari mgogoro huo ulifikishwa Taasisi ya Kuzuia na kupambana na kwamba wao kama wajumbe wa bodi wamekwisha kuhojiwa na PCCB.

Hata Spika wa jumuiya hiyo pia kahojiwa.

Inadaiwa kuwa ofisi ya spika wa jumuiya imetoa tangazo lililochapwa katika moja ya magazeti nchini.

Katibu wa Burunge WMA Benson Mwaise alikiri kuona tangazo la kutangazwa Kitalu hata hivyo alisema yeye kama Katibu ahusiki wala Bodi ya wadhamini ambao ndio wanamamlaka kisheria kutangaza.

Afisa Uhusiano wa EBN Charles Sylvester alisema wameshtushwa na Tangazo lililotolewa kwenye vyombo vya habari kuwa Kitalu kipo wazi na kwamba kampuni zitume maombi.

“Wakati sisi bado tupo na tuna vibali vyote halali pamoja na mikataba husika.”

“Tumeuliza WMA tumeelezwa ni uamuzi wa spika na tayari Bodi ya wadhamini ambao ndio wanamamlaka ya kutangaza Kitalu imekana kuhusika na tangazo hilo,” alisema

Alisema kwa zaidi ya miezi mitatu kumekuwepo na mgogoro ndani ya WMA kutokana na spika ambaye anatumiwa na kampuni Moja ya uwindaji kutaka kuvunja mkataba bila kufuata taratibu lakini pia kudaiwa kushawishi viongozi wengine WMA.

Alisema kampuni ambayo imewekeza katika eneo hilo imekuwa na manufaa makubwa kwa jamii ikiwepo ujenzi wa shule, kutoa usafiri wanafunzi, kutoa fedha vikundi vya wanawake,kufundisha ujasirimali na inatumia zaidi ya shilingi milioni 400 kila mwaka kupambana na ujangili.

Burunge WMA ina eneo la kilomita za mraba 283 ambapo kuna wawekezaji kadhaa wa Utalii na  EBN ndio mwekezaji mkubwa  ambaye ametoa ajira kwa zaidi ya watu 200 kutokana na kuendesha shughuli za Utalii wa picha na Kambi za Utalii na amekuwa na program za kupambana na ujangili.W

Habari Zingine

Maoni yamefungwa, lakini 0naweza kushea habari